Mgombea urais wa
chama cha Republican nchini Marekani Donald Trump amedai uchaguzi nchini
humo "unaibiwa" na vyombo vya habari pamoja na "kwenye vituo vya
kupigia kura" kumzuia kushinda.
Matamshi hayo yanaonekana
kukinzana na ya mgombea mwenza wake Mike Pence, ambaye awali aliambia
kituo cha runinga cha NBC kwa Bw Trump bila shaka atakubali matokeo ya
uchaguzi, licha ya "kuonewa" na vyombo vya habari.
Mshauri wa Bw Trump, Bw Rudy Giuliani pia amewatuhumu wanachama wa Democratic kwa "udanganyifu".
Kura za maoni zinaonesha kwamba Bw Trump anapoteza ushawishi katika majimbo mengi muhimu yanayoshindaniwa.
Hayo yakijiri, mgombea mwenza wa mpinzani wa Trump, mgombea wa
chama cha Democratic Bi Hillary Clinton, Bw Tim Kaine amejibu vikali
madai hayo ya Bw Trump kwamba kuna njama ya kuiba kura uchaguzini na
kusema ni mbinu tu za kutaka kuzua wasiwasi.
Bw trump ametilia shaka uhalali wa shughuli ya sasa ya uchaguzi kwenye msururu wa ujumbe kwenye Twitter.
Ameandika
hatimaye kwamba: "Uchaguzi huu bila shaka unaibiwa na wanahabari wasio
wa kweli na wa kupotosha ambao wanamtetea Hillary mwovu - lakini pia
katika vituo vingi vya kupigia kura - Inasikitisha."
Awali, Bw Trump alikuwa amewatuhumu wanahabari kwa kuchapisha habari za uongo.
"Uchaguzi
huu unaibiwa na wanahabari, kwenye juhudi za pamoja wakishirikiana na
wanakampeni wa Clinton, kwa kuchapisha habari za mambo ambayo hayajawahi
kutokea!"
Trump: Kura zinaibiwa vituoni Marekani
Reviewed by Mipiko
on
6:44 PM
Rating: 5