Breaking News

Kaimu meneja wa mradi wa maji awekwa ndani kwa saa 48




Mkuu wa wilaya ya Newala mkoani Mtwara Aziza Mangosongo amewaweka ndani  masaa 48 kaimu meneja wa mradi wa maji Makondeko mhandisi Athumani Semkondo  pamoja na msaidizi wake Mohameed Sabri kwa kosa la kuhujumu miundombinu ya maji na kusababisha vijiji zaidi ya 14 vyenye wakazi wapatao  elfu 60 kukosa maji kwa zaidi ya miaka mitano na hivyo kuwasabishia usumbufu mkubwa.
Akizungumza na waandishi wa habari mkuu wa wilaya ya Newala Aziza Mangosongo amesema ni jambo la kusikitisha kuona viongozi waliopewa dhamana na serikali wanakuwa sehemu ya kuhujumu umma ikiwa ni pamoja na kuzuia maji kwenda kwa wananchi na badala yake  kuyaelekeza kwa wafanyabiashara wa maji kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitano.
Akijitetea baada ya kutolewa ndani ya kituo cha Polisi meneja wa mamlaka ya maji Makonde Athumani Semkondo amekiri kuwapo kwa hujuma hiyo ambayo amesema huenda ilifanywa na watendaji wake wa chini pasipo yeye kujua.
Hata hivyo mkuu huyo wa wilaya anasema sehemu kubwa ya tatizo la maji katika wilaya ya Newala linasababishwa na urasimu, madhaifu ya viongozi na watendaji kutosimamia maadili ya kazi  zao.