Uvumi kuhusu kufariki kwa Rais Kiir wazua hali ya wasiwasi mjini Juba
Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir wakati wa mkutano na waandishi wa habari katika Ikulu ya rais mjini Juba, Julai 14, 2016.
Uvumi
kuhusu kufariki kwa rais wa Sudan Kusini Salva Kiir umesababisha hali ya
wasiwasi, Jumanne hii, Oktoba 12, katika mji mkuu wa Sudan Kusini,
Juba. Hata hivyo, hali katika nchi hiyo si nzuri. Tume ya Umoja wa
Mataifa nchini Sudan Kusini (UNMISS) imesema kuwa mauaji na mapigano
vinaendelea katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Wakazi wa
mji wa Juba walijiuliza Jumanne hii nini kinatokea. Askari walionekana
wengi katika mitaa mbalimbali ya mji mkuu wa Sudan Kusini, jambo ambalo
limeonekana si la kawaida, hasa karibu na wizara mbalimbali na Ofisi ya
rais. Uvumi ulielezea haraka kufariki kwa Rais Salva Kiir. Taarifa hii
ya kifo cha Rais Kiir ilirushwa kwenye mitandao ya kijamii.
Uvumi
ulizagazwa nchini kote hasa katika mji mkuu wa nchi hiyo, jambo ambalo
lilipelekea Michael Makuei, Waziri wa Mawasiliano na Msemaji wa serikali
kuingilia kati kwa kukanusha. Hiyo haikutosha, hali hii pia ilipelekea
Rais Kiir mwenyewe kuzunguka katika mitaa ya mji wa Juba. "Ah kumbe bado
hai," alishangaa mkazi mmoja wa mji wa Juba kwenye Twitter, akibaini
kwamba alimuona kwa jicho lake akiwa katika gari ndogo aina ya 4X4.
Hali hii
ya wasiwasi imeshuhudiwa, angalau katika mji mkuu. Kwa sababu hali ya
usalama mikoani bado ni mbaya. Tume ya Umoja wa Mataifa nchini Sudan
Kusini (UNMISS) imeelezea mapigano katika mji wa Leer, mji wa kaskazini,
na kumekua na visa vya mashambulizi ya kuvizia dhidi ya raia kwenye
barabara inayotokea katika mji wa Juba kuelekea kwenye mpaka na Uganda.