Breaking News

Ban Ki-moon afanya mazungumzo na rais mteule wa Gambia


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bw. Ban Ki-moon amefanya mazungumzo kwa njia ya simu na rais mtuele wa Gambia Bw Adama Barrow, na kumwambia kuwa Umoja wa Mataifa unaiunga mkono Gambia kufanya makabidhiano ya madaraka kwa wakati, kwa amani na utaratibu.

Bw Ban Ki-moon amempongeza Bw Barrow kwa ushindi wake katika uchaguzi wa urais, na kumtaka awahamasishe wafuasi wake wawe wavumilivu na waepuke kuzusha vurugu.

Bw Barrow ameshinda katika uchaguzi uliofanyika tarehe mosi mwezi huu, rais wa sasa Yahya Jammeh wa Gambia atakayemaliza muda wake tarehe 19 Januari mwakani alipinga matokeo siku chache baada ya uchaguzi huo. Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika Magharibi ECOWAS imeamua kutuma vikosi nchini Gambia ili kulinda usalama wa rais mteule, viongozi wa kisiasa na raia wa nchi hiyo.