Breaking News

  

WANANCHI WA MKOA WA KILIMANJARO WAOMBWA KUCHANGAMKIA HUDUMA YA TOTO AFYA KADI


Meneja wa mfuko wa bima ya Afya wa Taifa Bw.Fidelis Shauritanga

Meneja wa mfuko wa bima ya afya wa Taifa( NHIF )mkoa wa Kilimanjaro bw. Fidelis Shauritanga amewaomba wananchi wa mkoa huo kujiunga na huduma  mbalimbali za mfuko wa bima hiyo ili  kuboresha afya zao.

Akizungumza na Efm ofisini kwake mapema hivi leo amesema kuwa wananchi wa mkoa huo wamekuwa wakinufaika na huduma za mfuko wa bima ya afya wa taifa kupitia vituo vya serikali,taasisi na mashirika ya dini pamoja na vituo binafsi.

Amesema mpaka sasa mkoa wa Kilimanjaro vituo vilivyosajiliwa jumla yake ni 292,ambapo vituo vya serikali ni 192,mashirika na Taasisi za dini vikiwa ni 72 na vituo vya watu binafsi ni 24.

Hata hivyo amewahamasisha wananchi wa mkoa huo kujiunga na huduma ya toto afya kadi ambapo huduma hiyo  inamuwezesha mtoto wa umri chini ya miaka 18 kutibiwa nchi nzima kwa zaidi ya vituo vya afya 7000 ambavyo vimesajiliwa na mfuko huo kwa gharama ya shilingi 50400 kwa mwaka mzima.

Pia alieleza baadhi ya changamoto ambazo anakumbana nazo katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kutoka katika mfuko huo ikiwa ni pamoja na baadhi ya vituo vya afya kukosa vifaa tiba,madawa na miundombinu mibovu,

Sambamba na changamoto hizo amesema kuwa baadhi ya waajiri wamekuwa wakichelewesha michango ya wanachama jambo ambalo hupelekewa baadhi yao kukosa huduma kwa wakati pindi wanapohitaji msaada wa haraka.

Alieleza kuwa mfuko wa bima wa taifa unatoa huduma ya mikopo kwa riba nafuu hivyo ameziomba halmashauri za mkoa wa Kilimanjaro pamoja na wamiliki wa vituo vya afya kuweza kuchangamkia fursa ya mikopo hiyo ili kuboresha huduma katika vituo ambapo mikopo inayotolewa ni pamoja na madawa,vifaa tiba pamoja na mkopo kwa ajili ya kuboresha miundombinu ikiwemo majengo.


Amezitaja baadhi ya taasisi na mashirika ambayo yameweza kunufaika na mikopo hiyo ikiwa ni pamoja na KCMC Moshi,kituo cha afya Mawenzi pamoja na Same hospital.